Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban aziomba nchi wanachama kuunga mkono watu wa Palestina

Ban aziomba nchi wanachama kuunga mkono watu wa Palestina

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, ameziomba nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kuunga mkono juhudi za utafutaji suluhu la mataifa mawili ili kuutokomeza mgogoro kati ya Israel na Palestina.

Bwana Ban amesema hayo katika ujumbe wake wa Siku ya Kimataifa ya kusimama bega kwa bega na watu wa Palestina, ambayo ni leo Novemba 29. Bwana Ban amesema maadhimisho ya siku hii mwaka huu yanafanyika wakati washauri wa Israel na Palestina wanapofanya kazi pamoja ili kufikia lengo lililokubaliwa la suluhu la kina la amani kwa masuala yote yanayohusiana na utaifa.

Amesema pande zote zinatakiwa kutenda vitendo vinavyoonyesha kuwajibika, na kujiepusha na vitendo vyovyote vinavyoweza kuhatarisha matumaini ya kufanikiwa mazungumzo hayo.