Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IUCN yachukua hatua kudhibiti biashara haramu ya ngozi ya Chatu

IUCN yachukua hatua kudhibiti biashara haramu ya ngozi ya Chatu

Hofu juu ya kutoweka kwa aina kuu mbili za chatu Kusini Mashariki mwa Asia kumesababisha kuanzishwa kwa ubia kati ya shirika la kimataifa la uhifadhi, IUCN na kampuni ya KERING inayomiliki nembo ya GUCCI. Ubia huo ulioanzishwa na kituo ha kimataifa cha biashara, ITC unalenga kuhakikisha biashara endelevu ya ngozi ya nyoka huyo aina ya Chatu na kuhakikisha biashara yake inakuwa na manufaa kwa mapana zaidi. Mkuu wa kitengo cha biashara na mazingira ITC Alex Kasterine amewaambia waandishi wa habari mjini Geneva kuwa wazo la ubia huo linatokana na ripoti iliyochapishwa mwaka jana.

(Sauti ya Alex)

“Biashara ya ngozi ya nyoka ilionekana kuwa na thamani ya dola bilioni Moja kwa mwaka. Na kiasi kikubwa cha fedha hicho tumekadiria chatokana na biashara haramu kutokana na biashara ya magendo na ukiukwaji wa vibali vya CITES. Jambo lingine ni ukosefu wa uendelevu kwenye biashara hiyo., kwa hiyo kuna taarifa kidogo sana kuhusu idadi ya ngozi, idadi ya nyoka wanaokusanywa kutoka msituni, na iwapo idadi hiyo ni endelevu au la!Na hii ni muhimu kwa kuzingatia ongezeko la mahitaji ya bidhaa za anasa zitumiazo malighafi hiyo hususan mabegi na viatu.”

Amesema baada ya kuchapishwa kwa ripoti hiyo, KARENG-GUCCI walifuata IUCN kwa ajili ya ubia huo ambapo watafanya utafiti kwenye maeneo matano ikiwemo …..

(Sauti ya Alex)

“ ITC itahusika na kutambua athari za biashara ya chatu kwa maisha ya kila siku ya wakazi wa maeneo husika, hatufahamu idadi ya watu wanaoshiriki biashara hiyo lakini yasemekana ni mamia ya maelfu na wanaishi maeneo ya pembezoni kama vile misituni huko Kusini mashariki mwa Asia. Kwa hiyo twataka kufahamu bayonuai inawezaje kuchangia maisha ya wakazi hao. Wabia wengine watahusika na maeneo mengine kama vile kufuatilia ukamataji wa chatu ili kuimarisha upatikanaji endelevu na kuendeleza mazingira bora zaidi kwa nyoka hao na matunzo bora kwa wale wanaokamatwa.”