Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa OCHA ahitimisha tathmini ya janga la kimbunga huko Ufilipino

Mkuu wa OCHA ahitimisha tathmini ya janga la kimbunga huko Ufilipino

Mkuu wa Ofisi ya masuala ya kibinadamu kwenye Umoja wa Mataifa, OCHA, Bi. Valerie Amos amehitimisha tathmini yake ya usaidizi wa kibinadamu huko Ufilipino kufuatia janga la kimbunga Haiyan lililopiga nchi hiyo takribani wiki mbili zilizopita. Ripoti ya Assumpta Massoi inafafanua zaidi.

(Taarifa ya Assumpta)

Baada ya ziara ya wiki hii kwenye maeneo ya Tacloban, Roxas na Guiuan, Bi. Amos pamoja na kutoa pongezi kwa Ufilipino na wabia wa kimataifa kwa jinsi walivyochukua hatua za usaidizi, ameonya kuwa kuwa mbinu mbadala za usaidizi zahitajika ili kuweza kumfikia kila mhitaji.

Mathalani amesema msaada wa makazi ni dhahiri kwenye maeneo yaliyokumbwa na kimbunga na hata misaada ya dharura ili kuwezesha maisha yarejee katika hali ya kawaida na wananchi waendelee na shughuli za kuwaletea kipato kama vile kilimo. Amesema usaidizi kwa serikali hususan kwa mipango ya ujenzi baada ya kimbunga hicho ni muhimu kuzingatiwa.

Wakati hayo yakijiri Barbar Baloch wa Shirika la kuhudumia wakimbizi anapaza sauti za usaidizi wa makazi.

(Sauti ya Baloch)