Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama lalaani vikali shambulizi la bomu Lebanon

Baraza la Usalama lalaani vikali shambulizi la bomu Lebanon

Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, wamelaani vikali shambulio la bomu lililotekelezwa dhidi ya ubalozi wa Iran mjini Beirut, Lebanon, ambalo limewaua watu wapatao 23 na kuwajeruhi wengine zaidi ya 140 karibu na ubalozi huo.

Kundi moja linajihusisha na kundi la kigaidi la Al-Qaeda limedai kutekeleza shambulizi hilo.

Wanachama wa Baraza la Usalama wametuma risala za rambirambi kwa familia za wahanga na kuwapa pole wote walojeruhiwa, pamoja na watu na serikali za Lebanon na Iran. Ujumbe huo wa Baraza la Usalama umesomwa kwa waandishi wa habari na rais wa Baraza hilo kwa mwezi huu wa Novemba, Balozi Liu Jieyi wa Uchina.

“Wanachama wa Baraza la Usalama wamesisitiza kuwa ugaidi, uwe wa aina gain, ni mojawepo ya tishio kubwa zaidi kwa amani ya kimataifa na usalama, na kwamba vitendo vyovyote vya ugaidi ni uhalifu na hauwezi kukubalika, bila kujali kinachouchochea, unakotendeka, mahali unapotekelezwa, au anayeutekeleza. Wanachama wa Baraza la Usalama wamesisitiza haja ya kuwafikisha walohusika mbele ya sheria.”

Balozi Jieyi amesema wanachama wa Baraza la Usalama wamesisitiza haja ya kukabiliana na tishio linalosababishwa na ugadi kwa vyovyote vile, chini ya mkataba wa Umoja wa Mataifa na majukumu yote chini ya sheria za kimataifa.