Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuwalinda wakimbizi wa ndani Sudan Kusini kupewe kipaumbele:Beyani

Kuwalinda wakimbizi wa ndani Sudan Kusini kupewe kipaumbele:Beyani

Hatua za kibinadamu, kujumuishwa katika katiba, maendeleo na hatua za kuleta amani ni viungo muhimu kwa suluhu ya wakimbizi wa ndani na wale wanaorejea nyumbani. Hayo yamesemwa na mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu za wakimbizi wa ndani Chaloka Beyani ambaye ameongeza kuwa maendeleo na amani haviwezi kupatikana wakati maelfu ya Wasudan Kusini wanaendelea kutawanywa.

Beyani alikuwa ziarani Sudan Kusini kuanzia Novemba 6 hadi 15. Amesema wakati jimbo la Jonglei ndio linalohifadhi idadi kubwa ya wakimbizi wa ndani lakini ni suala linalojitokeza nchi nzima na hivyo ni lazima lishughulikiwe kama wajibu wa kitaifa.

Amesema ukimbizi wa ndani unasababishwa na vita vya silaha, migogoro ya kikabila kutokuwepo na usalama, ukiukwaji wa haki za binadamu na pia majanga ya asili. Masuala ya kuhamishwa kwa nguvu pia yanaonekana kuchangia. Bwana Beyani amezungumzia pia hali ya wakimbizi hao wa ndani ya kushindwa kukabiliana na maisha , akiongeza kuwa wengi wao ama wanaogopa au hawawezi kupata huduma muhimu na misaada ya kibinadamu.