Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IAEA kujadili ongezeko la asidi baharini katika mkutano wa Warsaw

IAEA kujadili ongezeko la asidi baharini katika mkutano wa Warsaw

Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA, linaandaa mjadala kuhusu kuongezeka kwa viwango vya asidi baharini mnamo Novemba 18, pembezoni mwa mkutano wa kimataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi, ambao unaendelea mjini Warsaw, Poland.

Jopo la wataalam litajadili hali hii inayotia hofu kimataifa, na ambayo inahatarisha uhai wa viumbe wote wa baharini, na wote wanaoyategemea mabahari.

Mzingira ya majini yanayohakikisha uzuri wa mabahari yanapata shinikizo kubwa, kufuatia kuongezeka kwa viwango vya asidi kwa kasi ambayo haijawahi kushuhudiwa, wakati mabahari hayo yakichafuliwa na kaboni inayotokana na shughuli za mwanadamu.

Majadiliano ya mkutano huo yanatarajiwa kuangazia mikakati ya kukabiliana na changamoto hizi, ikiwemo haja ya kuwepo ufuatiliaji na uratibu zaidi wa kimataifa, kama vile wajibu wa Mtandao wa Kimataifa wa Kuangalia Kuongezeka kwa Asidi Baharini na mashirika mengine husika.