Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uzalishaji wa afyuni Afghanistan wapanda kwa asilimia 36

Uzalishaji wa afyuni Afghanistan wapanda kwa asilimia 36

Upandaji wa afyuni nchini Afghanistan ulipanda kwa asilimia 36 mwaka huu, ambacho ni kiwango cha juu zaidi, kwa mujibu wa ripoti ya utafiti katika upandaji mmea huo unaotumiwa kutengeneza dawa haramu za kulevya, ambayo imetolewa leo mjini Kabul na wizara ya kukabiliana na dawa za kulevya na ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na dawa hizo na uhalifu, UNODC.

Mkurugezi Mkuu wa UNODC, Yuri Fedotov, amesema hali hiyo inatia wasiwasi kwani inatishia afya, ustawi na maendeleo nchini Afghanistan na kimataifa.

Amesema kinachohitajika sasa ni mwitikio wa pamoja na wa kina kwa tatizo hilo, utakaojumuishwa katika ajenda endelevu ya usalama, maendeleo na ujenzi wa taasisi.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, eneo linakopandwa mmea huo iliongezeka kutoka ekari 154,000 mwaka ulopita, hadi ekari 209,000, na hivyo kuzidi kiwango cha juu zaidi kuwahi kurekodiwa cha ekari 193,000 mnamo mwaka 2007.

Wkaulima wengi wanavutiwa na mapato yatokanayo na mmea huo, kwani kilo moja ya afyuni inauzwa kwa dola 145, na thamani yake kwa ujumla ni dola milioni 950, ambayo ni asilimia 4 ya mapato ya kitaifa kwa ujumla.