Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Utashi na uzingativu wa serikali unaweza kukabiliana na ukatili wa kingono DRC: Bangura

Utashi na uzingativu wa serikali unaweza kukabiliana na ukatili wa kingono DRC: Bangura

Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu ukatili wa kingono katika maeneo ya vita, Zainab Hawa bangura, amekaribisha tangazo la Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, DRC la hatua mpya za kukabiliana na ukatili wa kingono nchini humo.

Ameelezea pia kufurahishwa na tangazo la Rais Kabila la Oktoba 23 kwa wabunge kuwa ameamua kumteua mwakilishi wake kuhusu ukatili wa kingono na usajili wa watoto katika vita vya silaha.

Bi Bangura amemwomba Rais Kabila kumteua afisa huyo wa ngazi ya juu haraka iwezekanavyo, huku akiahidi uungwaji mkono wa dhati kutoka kwa Umoja wa Mataifa kwa jukumu hilo muhimu.

Bi Bangura pia amesema kuwawajibisha watu kwa makosa ya ukatili wa kingono ni muhimu katika kuzuia uhalifu huo, na kukaribisha tangazo la kutowajumuisha wahalifu wa ukatili wa kingono katika msamaha wa rais wa jumla kwa wafungwa.