WHO yatoa huduma kwa waathiriwa wa tufani nchini Ufilipino
Shirika la afya duniani WHO limendaa mikakati kwa ushirikono na idara ya afya nchini Ufilipino katika jitihada za kuwasaidia wale walioathiriwa na tufani Haiyan.
Tufani inayofahamika miongoni mwa wenyeji kama Yolanda ilikumba eneo la kati la Archipelago siku ya Ijumaa asubuhi ikiwa na upepo uliovuma kwa kasi ya kilomita 250 kwa saa. Watu wanaoishi kwenye maeneo yaliyoathiriwa walijeruhiwa huku vituo vya afya vikisalia vimeharibiwa. Kutoka na hali hiyo huduma za afya kwenye maeneo yaliyoathiriwa zimetatizwa pakubwa. Mwakilishi wa WHO nchini Ufilipino Dr Julie Hall anasema kuwa WHO inashirikiana kwa karibu na serikali ya Ufilipino kwenye mikakti ya kuokoa maisha na kuwahudumia wale walioathiriwa na gharika hiyo. Serikali ya Ufilino inakadiria kuwa watu milioni 4.5 wameathiriwa katikati mwa Ufilipino na sasa WHO inakusanya misaada kuisaidia serikali kutoa huduma za dharura.