Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waathirika wa kimbunga Haiyan Ufilipino wasaidiwe :Amos

Waathirika wa kimbunga Haiyan Ufilipino wasaidiwe :Amos

Mratibu mkuu wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura wa Umoja waMataifa Bi Valarie Amos amesema amestushwa sana na ripoti za vifo vya watu na uharibifu mkubwa uliosababishwa na kimbunga Haiyan au Yolanda huko Ufilipino. Amesema kuna idadi tofauti ya waliopoteza maisha ikiwemo ile ya chama cha msalaba mwekundu ambayo kwa sasa ni 1200, na kuna hofu ya idadi hiyo kuongezeka.  Kwa mujibu wa serikali ya Ufilipino takriban watu milioni 4.3 wameathirika katika majimbo 36 na tathimini ya awali inaonyesha kwamba maelfu ya nyumba zimebomolewa, barabara hazipitiki na watu wanahitaji haraka chakula, maji, malazi na umeme. Serikali imeshaweka makazi ya muda na kutuma helkopta ambazo zinasambaza mahitaji muhimu huku ikiongeza juhudi za kuwasaka na kuwaokoa wengine. Mashirika ya Umoja wa mataifa nchini humo na washirika wao wa masuala ya kibinadamu wanaisaidia serikali ya Ufilipino katika operesheni za uokozi na kutathimini hali pamoja na kukimbiza haraka mahitaji ya muhimu. Bi Amos amesema amepeleka timu kubwa ya Umoja wa Mataifa ya majanga na tathimini, UNDAC ambapo baadhi yao wamewssili leo Tacloban moja ya maeneo yaliyoathirika vibaya katika jimbo la Leyte.