Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uchina yachangia dola milioni 2 kufadhili huduma za WFP Syria

Uchina yachangia dola milioni 2 kufadhili huduma za WFP Syria

Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China imetoa mchango wa dola milioni mbili kwa ajili ya huduma za dharura za Shirika la Mpango wa Chakula Duniani, WFP, ambalo sasa linawasaidia watu wapatao milioni nne ndani ya Syria waloathiriwa na mzozo.

Mchango huo utaisaidia WFP kununua tani 2,000 za ngano, mafuta ya kupikia, na mchele, ambavyo vitasambaziwa watu wapatao milioni 1.2, ambao wamelazimika kuhama makwao kutokana na mapigano, na hivyo kukidhi mahitaji yao ya chakula ya mwezi mzima.

WFP imetoa shukrani za dhati kwa serikali ya Uchina, ikisema kuwa mojawapo ya changamoto inazokumbana nazo katika kutaka kuwafikishia waathiriwa wa mzozo chakula ni uhaba wa fedha za kununua chakula hicho mapema.

Utoaji misaada nchini Syria ndiyo shughuli kubwa zaidi, na pia kanganishi zaidi ya WFP kote duniani. WFP inahitaji dola milioni 30 kila wiki ili kukidhi mahitaji ya watu waloathiriwa na mzozo wa Syria.