Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nchi za Afrika hazitoi ushirikiano wa kutathmini hali ya haki za binadamu: Kiai

Nchi za Afrika hazitoi ushirikiano wa kutathmini hali ya haki za binadamu: Kiai

Mtaalam maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki ya kufanya mikutano ya amani na haki ya kujumuika, Maina Kiai, ametoa wito kwa nchi za Afrika zishirikiane naye na wenzie katika kufanya tathmini ya hali ya haki za binadamu katika nchi hizo.

Katika mahojiano na Redio ya Umoja wa Mataifa, Bwana Kiai, amesema katika muktadha wa uchaguzi, haki za watu hukiukwa kote duniani, lakini ulimwengu huangazia tu siku ya uchaguzi yenyewe, na mara nyingi kutangaza kuwa uchaguzi umekuwa huru na wa haki, bila kuangalia ikiwa vyama vya upinzani vinaruhusiwa kufanya mikutano au mashirika ya umma kushiriki ipasavyo.

Akiangazia nchi za bara la Afrika, amesema wataalamu wa haki za binadamu wanapata changamoto kubwa, kwani mara nyingi nchi hizo hazitoi mwaliko wowote kwao kwenda kukagua hali ya haki za binadamu.