Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dola Milioni 46.8 zahitajika kusaidia wahanga wa tetemeko la ardhi ufilipino: OCHA

Dola Milioni 46.8 zahitajika kusaidia wahanga wa tetemeko la ardhi ufilipino: OCHA

Mashirika ya misaada yametoa ombi maalum la dola Milioni 46.8 kusaidia maelfu ya wahanga wa tetemeko la ardhi lililokumba Ufilipino siku Kumi zilizopita. Tetemeko hilo kwenye kisiwa cha Bohol lilisababisha vifo vya watu 201 huku zaidi ya Laki Tatu wakipoteza makazi au kulazimika kuhama ambapo msemaji wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada, OCHA Jens Learke anasema mahitaji yao ni makubwa. Mathalani amesema kimbunga pepo za kaskazini mashariki kitaendelea kupiga eneo hilo la Bohol hadi mwezi Disemba na hivyo watu kuwa hatarini zaidi na kukosa pahala pa kulala. Amesema watu hao wanahitaji malazi ya muda na suala lingine ni maji safi na salama pamoja na umeme ambavyo vimekatika kutokana na tetemeko hilo. OCHA inasema ni matarajio yake kuwa ombi hilo litaitikiwa na kuwezesha mashirika ya misaada kutia shime jitihada za usaidizi zilizoanza kufanywa na serikali ya Ufilipino hususan kwa makundi maalum ya wanawake na watoto.