Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuibuka malaria isotibika ni jambo la kutia hofu: WHO

Kuibuka malaria isotibika ni jambo la kutia hofu: WHO

Shirika la Afya Duniani, WHO limeonya kuhusu kuibuka kwa aina ya ugonjwa wa malaria ambao hautibiki kwa dawa za malaria zilizopo, na kusema kuwa hali hiyo inazua changamoto kwa juhudi za kuzuia na kutokomeza malaria, na hivyo inapaswa kukabiliwa kama jambo la dharura. Joshua Mmali ana taarifa kamili.

(TAARIFA YA JOSHUA)

Aina ya ugonjwa wa malaria usotibika kwa dawa inayopendekezwa ya artemisinin ulithibitishwa kwanza kwenye mpaka kati ya Cambodia na Thailand mnamo mwaka 2008, na sasa umebainika katika nchi za Myanmar na Viet Nam. Kwa mujibu wa WHO, kuibuka kwa aina hii ya malaria kunaweza kuvuruga hatua zilizopigwa katika kuzuia na kutokomeza malaria, na hivyo kusababisha hatari kubwa kiafya duniani.

Dawa zenye artemisinin ndizo zinazotumika katika kutibu aina ya malaria iitwayo Plasmodium falciparum, ambayo hupatikana katika nchi nyingi ambako ugonjwa huo hupatikana, na zimechangia kwa kiasi fulani katika kupunguza mzigo wa malaria kote duniani.

Ugonjwa wa malaria unaathiri mno bara la Afrika, lakini pia unapatikana katika nchi kumi kati ya nchi 37 kwenye eneo la magharibi ya bahari ya Pasifiki, kama vile Uchina, Cambodia, Malasyia, Ufilipino, Jamhuri ya Korea, na nyinginezo.