Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Sheria za kipindi cha mpito ni lazima zizingatie kanuni za kimataifa za haki: Pillay

Sheria za kipindi cha mpito ni lazima zizingatie kanuni za kimataifa za haki: Pillay

Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu katika Umoja wa Mataifa, Navi Pillay, amesema kulinda haki za wanawake katika mazingira ya mizozo bado ni changamoto kubwa. Bi Pillay amesema hayo wakati akilihutubia Baraza la Usalama kwa njia ya video kutoka Geneva, baada ya wanachama wa baraza hilo kupitisha azimio la kuwajumuisha wanawake katika kuzuia na kutatua mizozo.

Mbali na kuzungumzia ujumuishaji wa wanawake katika kuhakikisha haki katika kipindi cha mpito na haki zao katika mizozo, Bi Pillay pia amezungumza kuhusu haja ya kuwepo uwajibikaji kwa uhalifu wanaotendewa wanawake. Amesisitizia pia thamani ya mikakati ya kina inayozingatia haki za binadamu katika harakati za kutekeleza haki wakati wa mpito.

Ameongeza kuwa juhudi zote za kuendeleza amani na haki ya mpito zinatakiwa zizingatie kanuni na viwango vya kimataifa vya haki za binadamu, ukiwemo Mkataba wa Kutokomeza Ubaguzi dhidi ya Wanawake, CEDAW.

(NAVI PILLAY)

“Kuweka misingi ya harakati za uongozi wa kisheria na haki ya mpito ni muhimu katika kuhakikisha uwajibikaji, na kuleta haki, ukweli na malipo ya fidia kwa uhalifu wanaotendewa wanawake. Ni muhimu pia katika kuzuia kuendeleza uhalifu kama huo siku zijazo. Kujumuishwa kuwajumuisha wanawake kikamilifu, kwa uhuru na uelewa katika mashauriano ya kitaifa kunaendelea kuchukuliwa kama muhimu katika kubuni na kutekeleza mikakati ya kina, inayoendana na muktadha na kujali mahitaji ya kijinsia katika haki ya mpito.”