Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kazi ya kuhamisha wakimbizi wa DR Congo huko Uganda yakamilika

Kazi ya kuhamisha wakimbizi wa DR Congo huko Uganda yakamilika

Shirika la Umoja wa Mataifa kuhudumia wakimbizi, UNHCR limekamilisha kazi ya kuwahamisha zaidi ya wakimbizi Elfu nane kutoka ardhi inayozozaniwa kati ya serikali yaUganda na wananchi kwenye kambi ya wakimbizi ya Kyangwali. John Kibego wa redio washirika ya Spice FM, anaripoti kamili kutoka Uganda.

 (Taarifa ya John Kibego)

Walioathiriwa ni wakimbizi waliotoroka mapigano nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), mnamo mwezi July na kufikishwa kwenye kambi ya wakimbizi ya Kyangwali mwezi Agosti. Lakini kabla ya kupata makazi, ilibidi serikali ifurushe maelfu ya wananchi waliodaiwa kuvamia eneo la wakimbizi. Hatimaye ufurushwaji wao ukaanza. Wiki tatu badaye wizara ya kushughulikia majanga ikaingilia kati na kuamrisha waliokuwa wamefurushwa warejee kwenye ardhi zao, na wakimbizi wakaelekezwa kwenye ardhi mbadala, karibu kilomita tisa kutoka hapo.

Collin Ote, afisa wakutetea wakimbizi kutoka ofisi ya shirika la kuhudumia wakimbizi la UNHCR ya Hoima anasema kuhamisha wakimbizi hao kumemalizika lakini kuwaingiza gharama ambazo hazikutarajiwa.

(Sauti ya Collin Ote)

Ufurushwaji wa wananchi wanaodaiwa kuingilia kambi hiyo ulipingwa mwanzoni na wanasiasa wa mitaa na wabunge kutoka eneo hili, wakitaka serikali ifungwe mipaka ya eneo la wakimbizi ili kubaini mvamizi na yule asiye mvamizi wa ardhi hiyo.

Douglas Asiimwe, afisa mwandamizi wa kutetea wakimbizi kutoka ofisi ya Waziri Mkuu amekuwa akiwalaani baadhi ya wanasiasa kwa madai ya kuvuruga juhudi za kufurusha wavamizi wa ardhi hiyo ya kambi ya wakimbizi yenye hati miliki yake

Kambi ya wakimbizi ya Kyangwali ni kubwa zadi kuliko zote humo nchin na kwa sasa ni nyumbani kwa zaidi ya wakimbizi elfu thelathini kutoka nchi zenye migogoro zikiwemo Somalia,Sudan na Jamhuri ya Kidemokrasia Congo (DRC).