Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IAEA yahitimisha ziara ya kukagua usalama wa nyuklia Marekani

IAEA yahitimisha ziara ya kukagua usalama wa nyuklia Marekani

Timu ya wataalam wa usalama wa nguvu za nyuklia ikiongozwa na Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA, imekamilisha leo ziara ya ukaguzi wa usalama wa mitambo ya umma inayotumia nguvu za nyuklia, na ambayo imepewa vibali na mamlaka ya kudhibiti nyuklia hapa Marekani, NRC.

Ukaguzi huo wa wiki mbili, ambao umefanywa kufuatia ombi la serikali ya Marekani ulirejelea mikakati ya kisheria na udhibiti nchini Marekani, ambayo inahusiana na usalama wa nguvu za nyuklia.

Timu hiyo iloongozwa na John O’Dacre wa Canada na ambayo imejumuisha wataalam wengine kutoka nchi nane wanachama wa IAEA, ilikutana na maafisa wa NRC na kukagua mifumo ya kulinda usalama kwenye Kituo cha Utafiti wa Nyuklia, NCRC.

Timu hiyo imehitimisha kuwa usalama wa nyuklia nchini Marekani ni mzuri na endelevu, na umeboreshwa kwa kiasi kikubwa katika miaka michache ilopita, na kutoa mapendekezo kuhusu jinsi ya kuendelea kuboresha usalama wa nyuklia kwa ujumla.