Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wasisitiza amani Sudan na Sudan Kusini ili kufanikisha chanjo ya polio

UM wasisitiza amani Sudan na Sudan Kusini ili kufanikisha chanjo ya polio

Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa limeitaka serikali ya Sudani na kundi la Sudan People’s Liberation Movement-North (SPLM-N kumaliza tofauti zao ili kuwezesha kampeni ya chanjo dhidi ya polio inayotarajiwa kuanza Novemba tano mwaka huu chini ya mashirika matatu ya Umoja huo lile la uratibu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu (OCHA), la kuhudumia watoto ,UNICEF pamoja na shirika la afya duniani ,WHO.

Taarifa ya baraza hilo iliyotolewa leo inasema hii inafuatia taarifa ya kukithiri kwa ugonjwa huo nchini Sudan na Sudan Kusini na pembe ya Afrika kwa ujumla ambayo imewasilishwa kwa pamoja na msaidizi wa katibu mkuu wa UM anayeshughulikia maswala ya kulinda amani Hervé Ladsous na kamanda mkuu wa kikosi cha UM cha amani ya mpito Abyei UNISFA, Meja Jeneral General Yohannes Tesfamariam wakati wakilieleza baraza la usalama hali katika nchi hizo mbili.

Kwa mujibu wa OCHA tishio la polio linaathiri zaidi ya watoto laki moja na elfu sitini na tano kwa zaidi ya miaka miwili sasa, ambapo ikiwa juhudi za kukomesha hazitachukuliwa ugonjwa huo utasambaa zaidi.

Baraza la usalama pia limesissitiza kuunga mkono utokomezaji wa polio katika maeneo hayo na kumtaka katibu mkuu wa UM kushirikiana na pande hizo kinzani katika kuhakikisha utekelezaji wa chanjo dhidi ya polio Sudan na Sudan Kusini.