Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanachama wa Baraza la Usalama wazuru ukanda wa Maziwa Makuu

Wanachama wa Baraza la Usalama wazuru ukanda wa Maziwa Makuu

Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, wamo ziarani kwenye ukanda wa Maziwa Makuu, ambako tayari wamezuru Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, DRC na Rwanda, kabla ya kuwasili nchini Uganda. Joshua Mmali na taarifa kamili

(TAARIFA YA JOSHUA)

Kabla ya kuondoka mjini Goma DRC Jumapili jioni na kuelekea Kigali, Rwanda, wanachama hao wa Baraza la Usalama wameunga mkono kujitoa kwa DRC katika kuendeleza harakati za amani zilizoanzishwa kupitia makubaliano ya mwezi Februari mjini Addis Ababa.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye uwanja wa ndege mjini Goma, Mwakilishi wa Kudumu wa Morocco kwenye Umoja wa Mataifa, Mohammed Loulichki, amesema mataifa mengine kwenye ukanda wa Maziwa Makuu pia yanapaswa kutimiza ahadi zao za kuendeleza harakati hizo za amani

Uhakika ni kwamba ujumbe tutakaopeleka kwa nchi hizo zingine ni sawa na ule tuliotoa hapa kwamba kuna ahadi zilizofanywa hapa ambazo baraza la usalama na jumuiya ya kimataifa wanangojea zitimizwe na zitekelezwe kikamilifu, kwa sababu hiyo ndio njia pekee ambapo pande zote husika zitaweza kuchangia kurejesha amani na utulivu ili kuhakikisha kuwa eneo hili litarejelea tena wajibu wake sio tu wa kuhakikisha amani ya ukanda mzima lakini pia wa kuhakikisha maendeleo ya kiuchumi”

Baada ya Rwanda na Uganda, wanachama hao wa Baraza la Usalama wanatarajiwa kuelekea mjini Addis Ababa, Ethiopia, kwenye makao makuu ya Muungano wa Nchi za Afrika, AU.