Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Sudan yatakiwa kuwafungulia mashtaka waandamanaji au iwaachie huru mara moja

Sudan yatakiwa kuwafungulia mashtaka waandamanaji au iwaachie huru mara moja

Nchini Sudan, ni zaidi ya wiki moja sasa tangu mamia ya wananchi waandamane kupinga kuondolewa ruzuku kwenye mafuta ya petroli kitendo kilichosababisha idadi kadhaa kukamatwa na kutiwa nguvuni. Hiyo ni kwa mujibu wa mtaalamu huru wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu nchini Sudan Mashood Adebayo Baderin.  Baderin ametaka serikali iamue moja ama kuwafungulia mashtaka au kuwaachia huru mara moja na kuacha kitendo cha kudhibiti vyombo vya habari. Bederin amesema waandamanaji wanashikiliwa bila taarifa yoyote na hawana fursa ya kuonana na mawakili au familia zao. Habari zinasema kuwa wanaharakati 800 ikiwemo wafuasi wa vyama vya upinzani na waandishi wa habari wamekuwa rumande kutokana na maandamano ambapo yasadikiwa watu 50 wameuawa na vikosi vya usalama. Maandamano ya kupinga kuondolewa kwa ruzuku kwenye mafuta ya petroli yalianza tarehe 23 mwezi uliopita kwenye jimbo la kati la Gezira na kuenea maeneo mengine ya Sudan ikiweko Khartoum, Omdurman, Darfur na Sudan Mashariki.