Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Viongozi wa dunia wataka ushirikiano katika mapambano dhidi ya malaria

Viongozi wa dunia wataka ushirikiano katika mapambano dhidi ya malaria

Viongozi wa dunia wamekusanyika pamoja kandoni mwa mkutano wa 68 wa baraza kuu la Umoja wa Mataifa kuzindua mbinu mpya ya kupambana na malaria ugonjwa ambao licha ya juhudi za kuutokomeza bado unaua takribani watu laki sita kila mwaka na hivyo kuwa changamoto kubwa ya maendeleo.

Mashirika makuu ya kupambana na maleria lile la kurudisha ugonjwa huo  RBM na  mpango wa maendeleo wa UM ,UNDP, yametaka ushirikiano wa pamoja katika sekta mbalimbali wa kutokomeza malaria ugonjwa ambao unaongoza kwa kusababaisha vifo kwa nchi za kusini  mwa Jangwa la Sahara.

Mkakati huo unaainisha hatua dhidi ya malaria kijamii na mazingira na unataka mikakati mipya dhidi ya ugonjwa huo isukumwe na mbinu ya maendeleo ya kimataifa kwa kuchagiza watunga sera na watendaji kuongeza ushirikiano kati ya sekta na kuongeza kasi ya kupambana na maleria kijamii na kiuchumi.

Katika mkutano huo Mkuu wa UNDP Rebeca Grynspan amesema ugonjwa wa maleria unahusiana na ukosefu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi ,umaskini kubaguliwa na kunyonywa akiongeza kuwa sekta ya afya ina wajibu katika hili na hivyo muitikio wa sekta mbalimbali ni muhimu ili dunia iondokane na mzigo wa malaria.

Kwa upande wake Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete amesema huu ni wakati mgumu  kwa Afrika ambayo inaweza kurudi nyuma au kuamua kutumia mtaji wa mafanikio yaliyofikiwa miaka ya nyuma. Ameongeza kuwa ili kuendeleza mafanikio hayo sekta zote za maendeleo na udhibiti wa mazingira zinahitajika