Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mzozo nchini CAR watishia usalama wa watoto: UNICEF

Mzozo nchini CAR watishia usalama wa watoto: UNICEF

Takribani watoto 3,500 wametumikishwa katika vikundi mbali mbali vyenye silaha huko Jamhuri ya Afrika ya Kati, na hiyo ni kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF. Shirika hilo linasema jeshi la serikali na vikundi vya waasi vimekuwa vikitumikisha jeshini watoto wa kike na wa kiume tangu kuanza kwa mzozo huo wa kisiasa mwezi Disemba mwaka jana. UNICEF inasema matumizi ya watoto ni uhalifu wa kivita likiongeza kuwa kwa sasa linawasiliana na vikosi vya serikali an waasi ili watoto hao waweze kuachiliwa huru. Marixie Mercado, msemaji wa UNICEF anasema mzozo huo umetikisa zaidi watoto na wengi wao hawawezi kupata huduma za afya huku kitisho cha ndoa za mapema kwa mtoto wa kike kikiwa dhahiri.

(Sauti ya Marixie)

“Mlipuko wa surua umeripotiwa karibu kila mahali nchini humu na hilo ni kwa sababu ya kuparaganyika kwa mfumo wa utoaji chanjo. Takrbani asilimia 60 ya shule bado zimefungwa kutokana na ghasia na walimu hawapo. Tishio la ndoa za lazima kwa watoto wa kike linaongezeka na watoto wengi wanaonyesha dalili za kupata msongo wa kisaikolojia. Kabla kuanza mzozo Disemba 2012 UNICEF ilikadiria watoto 2000 kutumikishwa na vikundi vyenye silaha lakini sasa kwa kuwa kila upande unatumikisha, tunakadiria kuna watoto 3500 kwenye vikundi hivyo.”

UNICEF inaandaa kampeni ya chanjo ya polio kuanzia tarehe 30 mwezi huu ikilenga watoto 750,000 walio hatarini kupata ugonjwa huo wakati huu ambapo WFP inaimarisha kampeni ya kusambaza misaada.