Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

ICC yaonya kuhusu ushawishi na kuweka hadharani mashahidi

ICC yaonya kuhusu ushawishi na kuweka hadharani mashahidi

Jaji wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC, ambaye anaisikiliza kesi dhidi ya Makamu wa Rais wa Kenya, William Samoei Ruto na mtangazaji Joshua Arap Sang, ametoa taarifa ya kukumbusha kuhusu umuhimu wa kuwalinda mashahidi na kuonya kuwa vitendo vyovyote ambavyo vitazuia upatikanaji wa haki vitakabiliwa kisheriaa.

Akiongea mwanzoni mwa kikao cha mchana cha kusikilizwa kesi hiyo, Jaji Chile Eboe-Osuji amesema kuwa ni hatia dhidi ya utekelezaji wa sheria katika mahakama ya ICC chini ya Mkataba wa Roma kwa mtu yeyote kufanya kitendo chochote ambacho kinaweza kumshawishi shahidi kwa njia ya rushwa, au kuzuia kuhudhuria kwa shahidi kwa kikao, au kutoa ushahidi, au kumuadhibu shahidi kwa kutoa ushahidi mahakamani.

Kwa mujibu wa kifungu cha 70 cha Mkataba wa ICC, mtu yeyote anayefanya kosa hilo anaweza kupewa kifungo cha hadi miaka mitano.

Jaji Eboe-Osuji ameongeza kuwa kitendo kama hicho pia kinaweza kutafsiriwa kama dharau kwa mahakama, na kusema kuwa kumweka hadharani shahidi ambaye amefichwa na mahakama pia ni hatia chini ya mahakama ya ICC.