Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Somalia bado kuna changamoto lakini hatukati tamaa: Kay

Somalia bado kuna changamoto lakini hatukati tamaa: Kay

Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Nicholas Kay amehutubia baraza la amani na usalama la Umoja wa Afrika huko Addis Ababa,Ethiopia na kueleza kuwa takribani mwaka mmoja tangu kuundwa kwa serikali yaSomalia, bado changamoto ya usalama inakabili nchi hiyo.  Bwana Kay amesema eneo lenye utata zaidi ni Kusini mwaSomaliahususan mji mkuu Mogadishu akitolea mfano matukio ya mashambulizi wakati wa mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani.  Hata hivyo amesema licha ya changamoto hizo, kurudi ni nyuma ni kamwe na ni lazima kukumbuka nchi hiyo ilikotoka akitoa shukrani za dhati kwa walinda usalama ambao wamejitoa mhanga kulinda raia vikiwemo vikosi vya Umoja wa Afrika nchini humo, AMISOM, jeshi la Ethiopia na jeshi laSomalia.  Bwana Kay amesema Katibu Mkuu anatambua changamoto ambazo AMISOM inakabiliana nazo ikiwemo kupanua wigo wa eneo la udhibiti na hivyo Umoja wa Mataifa uko tayari kuendelea kusaidia AMISOM hususan kuhakikisha inapata fedha za uhakika na za kutosha. Amesema Bwana Ban anaendelea kusihi Baraza la usalama kuzingatia suala hilo wakati huu ambapo shughuli ya kutathmini AMISOM ikianza leo hadi tarehe Sita mwezi ujao.