Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto milioni 3 nchini Syria wamesambaratishwa na vita

Watoto milioni 3 nchini Syria wamesambaratishwa na vita

Karibu watoto milioni 3 nchini Syria wamesambaratishwa na machafuko yanayoendelea nchini Syria kwa mujibu wa mashirika ya Umoja wa mataifa.

Shirika la Umoja wa mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR na lile la kuhudumia watoto UNICEF yanakadiria kuwa zaidi ya watoto milioni 2 wamekuwa wakimbizi wa ndani huku wengine milioni moja wamelazimika kuzikimbia nyumba zao na kuwa wakimbizi nje.

Zaidi ya nusu ya wakimbizi watoto wa Syria katika nchi jirani ni watoto  wa chini ya umri wa miaka 11. Mashirika hayo yanasema watoto wameathirika , wanamsongo wa mawazo na wanahitaji sababu za kuwapa matumaini.

Kamishina mkuu wa wakimbizi Antonio Guterres anasema maisha na usalama wa kizazi chote yapo katika hatihati akiongeza kuwa watoto wakimbizi wa ndani wanakabiliwa na hatari ya kuingizwa kwenye ajira ya watoto, dhuluma za kingono na usafirishaji haramu wa watu.

Ombi la kikanda la dola bilioni 33 ili kushughulikia mahitaji muhimu ya wakimbizi mpaka Desemba , hadi sasa limepata asilimia 38 tuu ya fedha zinazohitajika.