Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban aisifu Pakistan kwa mchango wake katika shughuli za ulinzi wa amani

Ban aisifu Pakistan kwa mchango wake katika shughuli za ulinzi wa amani

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, amelisifu taifa la Pakistan kwa kuwa nambari moja katika nchi zaidi ya mia moja zinazochangia vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa.

Bwana Ban ambaye yuko ziarani Pakistan, amesema hayo leo wakati wa kukizindua Kituo cha Kimataifa cha Amani mjini Islamabad, na kusifu mchango wa Pakistan katika mkutano wa Baraza la Usalama ulopitisha azimio la kuundwa kwa brigedi ya ulinzi mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, DRC.

Bwana Ban pia amezungumza kwenye Chuo cha Wasichana cha Islamabad, ambako amesisitiza umuhimu wa elimu katika maisha ya watu na kwa mataifa, akitoa mfano wake mwenyewe alipokuwa mdogo na ule wa msichana wa Kipakistani, Malala Yousafzai, ambaye amemsifu kwa hotuba yake yenye mafunzo kwenye Umoja wa Mataifa mnamo Julai 12, 2013.