Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa wasikitishwa na kurejea kwa sheria ya hukumu ya kifo Viet Nam

Umoja wa Mataifa wasikitishwa na kurejea kwa sheria ya hukumu ya kifo Viet Nam

Ofisi ya Haki za Binadamu katika Umoja wa Mataifa imeelezea kusikitishwa na kurejeshwa kwa utekelezaji wa hukumu ya kifo nchini Viet Nam kwa kuwanyonga mwanamume mmoja mwenye umri wa miaka 27 mjini Hanoi Agosti 6, kwa kumdunga sindano ya sumu.

Msemaji wa ofisi hiyo, Cecil Pouly amesema, mauaji hayo ambayo yamefanyika miezi 18 tangu mauaji mengine kuripotiwa kutekelezwa, yanawasilisha kurudi nyuma kwa taifa la Viet Nam katika sifa za ulinzi wa haki za binadamu. Ofisi ya haki za binadamu pia imeelezea hofu yake kuwa wafungwa wengine wapatao 116 huenda wakanyongwa, kwani sasa maombi yao yote ya rufaa yamekataliwa.

Mwezi uliopita, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu, Navi Pillay, alimwandikia Waziri Mkuu wa Viet Nam akisema kuwa nchi hiyo bado inashikilia hukumu ya kifo kwa makosa fulani ambayo hayafai kuadhibiwa kwa hukumu ya kifo, na kuomba hukumu hiyo iondolewe katika sheria zake.