Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Huenda ngamia ndio wanaoambukiza virusi vya Corona: WHO

Huenda ngamia ndio wanaoambukiza virusi vya Corona: WHO

Timu ya wanasayansi wa kimataifa imegundua kuwa huenda ngamia ndio wanaoambukiza wanadamu virusi hatari vya homa ya Corona, ambayo imewaathiri watu hasa katika ukanda wa Mashariki ya Kati. Hata hivyo, Shirika la Afya Duniani, WHO limesema kuwa ni mapema mno kutamatisha kuwa matokeo ya utafiti huo ni kamilifu kabisa.  Wanasayansi hao walichunguza sampuli za damu ilotolewa kwa mifugo, wakiwemo ngamia, kondoo, mbuzi na ng’ombe, kutoka nchi kadhaa tofauti. Mifugo hao walipimwa kuona ikiwa wana chembechembe za protini zinazozalishwa na mwili ili kutoa kinga dhidi ya maambukizi. Utafiti huo umeonyesha kuwa virusi vya Corona, au virusi vinavyofanana navyo vimekuwa vikienezwa miongoni mwa ngamia. Memsaji wa  WHO Tarik Jasarevic amesema ingawa matokeo ya utafiti huo yamekaribishwa, bado uchunguzi zaidi unatakiwa kufanyika.

Kile ambacho utafiti huu umeonyesha ni chembechembe za kinga katika ngamia. Inamaanisha kuwa ngamia hawa wameambukizwa awali, na hivyo kuzalisha hizo chembechembe za protini za kinga. Lakini ili kuhakikisha kuwa hivi virusi ni sawa na vile vinavyowaathiri wanadamu, tunatakiwa kupata virusi vyenyewe, na wala si chembechembe za kinga. Hiyo itakuwa hatua itakayofuata.