Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la usalama lalaani vikali shambulio la Jalalabad

Baraza la usalama lalaani vikali shambulio la Jalalabad

Wajumbe wa baraza la usalama wamelaani vikali shambulio la kujitoa muhanga  lililofanyika Jumapili Agosti 3 karibu na ubalozi wa India mjini Jalalabad,Afghanistan. Shambulio hilo limesababisha vifo kwa raia na kujeruhi watu wengine, wengi wakiwa ni watoto. Askari wa usalama wa Afghanistani ni miongoni mwa waliouawa katika shambulio hilo.

Wajumbe watoa salamu zao za rambirambi kwa familia za waliopoteza maisha, kujeruhiwa, kwa serikali na watu wa Afghanistan. Wajumbe wamesema vitendo vya ghasia dhidi ya ofisi za kibalozi havikubaliki na vinahatarisha maisha ya watu wasio na hatia licha ya kuvuruga utaratibu mzima wa kazi.

Wameongeza kuwa daima watasimama na watu wa Afghanistan katika kulinda uhuru wao na taasisi za serikali. Wajumbe hao pia wameelezea hofu yao dhidi ya tishio la Taliban, Al-Qaida na makundi mengine haramu yenye silaha . Wanataka wahusika wote ikiwa ni pamoja na waandaaji, watekelezaji na wafadhili wa vitendo ya kigaidi wafikishwe mahakamani.