Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

MONUSCO kutobadili msimamo kuhusu upokonyaji silaha

MONUSCO kutobadili msimamo kuhusu upokonyaji silaha

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kuweka utulivu huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, MONUSCU umesema haujabadilisha msimamo kuhusu uamuzi wake wa kufuwafuatilia wote walio na silaha haramu mjini Goma na maeneo jirani huko Kivu Kaskazini kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari. Msemaji wa MONUSCO, Luteni kanali Felix Basse ametoa kauli hiyo jumatatu Agosti Tano. Flora Nducha na taarifa kamili.

(TAARIFA YA FLORA NDUCHA)

Luteni Kanali Basse amesema kuwa hakuna wakati wowote ambapo kamanda wa kikosi amebadilisha mawazo na kwamba vikundi na watu binafsi wanaobeba silaha, ambao sio wanajeshi wala walinda usalama walipatiwa muda wa masaa 48 kusalimisha silaha.

Muda huo umeisha na kamanda amesema Monusco itaanza kutekeleza mifumo yote iliowekwa ili kuhakikisha usalama wa eneo hilo. Kwa hiyo ameongeza kuwa hakuna mabadiliko yoyote na wanaendelea na shughuli za kawaida ili kudumisha usalama.

Katika taarifa zilizotolewa na MONUSCO Jumatatu mpango huo umesema mtu yeyote ambaye sio sehemu ya vikosi vya kitaifa vya usalama na ambaye atapatikana na silaha Goma na maeneo yalio kaskazini mwa mji huo, atachukuliwa kama tishio kubwa kwa usalama wa raia.  Serikali ya DRC ilikubaliana na hatua za MONUSCO.