Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Punda, baiskeli vyatumika kubeba vilipukaji huko Afghanistan: UM

Punda, baiskeli vyatumika kubeba vilipukaji huko Afghanistan: UM

Kaimu msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayeongoza Idara ya Ulinzi na Usalama Kevin Kennedy amesema hali ya maisha ya kila siku huko Afghanistani ni ya hofu siyo tu kwa wananchi bali pia kwa wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa ambao kila uchwao hukutana na madhila yanayohatarisha usalama wao. Taarifa ya Alice Kariuki inafafanua zaidi.(Taarifa ya Alice)

Kennedy ambaye amerejea siku chache zilizopita kutoka Afghanistan ameiambia Radio ya Umoja wa Mataifa kwenye mahojiano maalum kuwa maisha ya kila siku yanaendelea kama kawaida iwe kwenye mji mkuu Kabul na miji mingine kama vile Kandahar lakini mazingira ya maisha na yale ya kazi kwa wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa na wananchi kwa ujumla ni magumu na ya hofu.

Amesema hali imekuwa ni ya hofu zaidi kutokana na maendeleo ya vifaa vinavyotumika kwenye milipuko kama vile wanyama, ambapo amesema kila siku kuna tukio la kuhatarisha usalama, liwe ni tukio dogo au kubwa.

 (SAUTI YA KENNEDY)

 Unapokuwa kwenye foleni barabarani, huna uhakika kama gari lililo pembeni yako ni  gaidi au vyovyote utakavyomuita. Na mbaya zaidi limebeba vilipukaji. Mbaya kuliko zote matukio siyo tu dhidi ya wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa bali pia  wafanyakazi wengine na wanamaji na vikosi vya NATO. Kulikuwepo Punda aliyebebeshwa vilipukaj. Sasa unapooona punda kwenye nchi hiyo ni kitu cha mwisho kabisa kudhani kuwa kinaweza kulipuka. Mbaya zaidi, baiskeli nazo zinawekewa milipuko, na ziko kila mahali na zinaweza kupita kando mwa magari na kuja karibu yako, kwa hiyo nafikiri kuna hofu ya usalama wa maisha ya watu.”

Hata hivyo Kaimu Mkuu huyo wa usalama na Ulinzi ndani ya Umoja wa Mataifa amesema licha ya hofu hiyo wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa wanafanya kazi kwa kujituma na wanachohitaji zaidi ni ushauri nasaha wa kuwawezesha kuendelea vyema zaidi na majukumu yao.