Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Serikali ya Madagascar yatakiwa kupiga vita biashara ya ngono dhidi ya watoto

Serikali ya Madagascar yatakiwa kupiga vita biashara ya ngono dhidi ya watoto

Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa Najat Maalla M’jid ametaka serikali ya Madagascar kufanya juhudi na kumaliza biashara ya watoto kwenye ukahaba na kuwalinda  watoto wote na dhuluma zingine zikiwemo kuuzwa kwa watoto na kuwafikisha mbele ya sheria wahusika.Bi Maalla M’jid alielezea hisia  zake kutokana na dhuluma hizo za biashara ya ngono kwa watoto na vile wahusika wanavyokwepa sheria. Mjumbe huyo maalum anasema kuwa umaskini kwa sasa unawaathiri karibu asilimia 92 ya watu wote nchini humo jambo ambalo limeathiri familia nyingi  na kuchangia kuongezeka kwa idadi ya watu wanaokosa kuhudhuria masomo na kujipata kwenye hatari ya kudhulumiwa kimapenzi.

Wakati wa ziara yake nchini Madagascar  iliyong’oa nanga tarehe 15 hadi 26 mwezi huu bi Maalla M’jid alikutana na viongozi kadha wa serikali  na pia wawakilishi kutoka  kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa na wanadiplomasia. Mjumbe huyo pia alikutana na watoto waathiriwa ambapo pia alizuru maeneo maarufu kwa vitendo hivyo.