Serikali ya Madagascar yatakiwa kupiga vita biashara ya ngono dhidi ya watoto
Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa Najat Maalla M’jid ametaka serikali ya Madagascar kufanya juhudi na kumaliza biashara ya watoto kwenye ukahaba na kuwalinda watoto wote na dhuluma zingine zikiwemo kuuzwa kwa watoto na kuwafikisha mbele ya sheria wahusika.Bi Maalla M’jid alielezea hisia zake kutokana na dhuluma hizo za biashara ya ngono kwa watoto na vile wahusika wanavyokwepa sheria. Mjumbe huyo maalum anasema kuwa umaskini kwa sasa unawaathiri karibu asilimia 92 ya watu wote nchini humo jambo ambalo limeathiri familia nyingi na kuchangia kuongezeka kwa idadi ya watu wanaokosa kuhudhuria masomo na kujipata kwenye hatari ya kudhulumiwa kimapenzi.
Wakati wa ziara yake nchini Madagascar iliyong’oa nanga tarehe 15 hadi 26 mwezi huu bi Maalla M’jid alikutana na viongozi kadha wa serikali na pia wawakilishi kutoka kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa na wanadiplomasia. Mjumbe huyo pia alikutana na watoto waathiriwa ambapo pia alizuru maeneo maarufu kwa vitendo hivyo.