Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto wanaathirika na vita DRC-UNICEF

Watoto wanaathirika na vita DRC-UNICEF

Mapigano yanayoendelea kati ya jeshi la serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC, dhidi ya kundi la waasi wa M23 na ADF Nalu katika eneo la Kivu Kaskazini Kivu yana madhara ya moja kwa moja kwa watoto katika eneo hilo. George njogopa na taarifa kamili.

(SAUTI YA GEORGE)

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF limesema kuwa limepokea taarifa kuhusiana na kuuwawa kwa watoto  pamoja na wale waliojeruhiwa ikiwa ni matokeo ya  machafuko ya hivi karibuni.

 Ripoti zinasema kuwa wakati idadi ya watoto wanaoathiriwa na machafuko hayo ikizidi kuongezeka, kuna wasiwasi mkubwa unaojitokeza kuhusiana na mustakabala wa eneo hilo.

Mwakilishi wa UNICEF nchini Congo Barbara Bentein amezitaka pande zinazopigana kwenye machafuko hayo kuhakikisha inawalinda watoto.

Ameongeza kuwa,wahusika kwenye machafuko hayo wanapaswa kutambua kuwa wanawajibu wa kujiepusha na vitendo vyovyote vinavyoweza kuathiri maisha ya raia.

Shirika hilo la Umoja wa Mataifa linakadiria kuwa, kiasi cha watoto 2,000 wanatumikishwa kama askari kwenye maeneo ya vita, na hali hiyo imedhihirika zaidi katika Jimbo la Kivu ya Kaskazini.