Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa WFP asifu juhudi za maendeleo vijijini nchini Rwanda

Mkuu wa WFP asifu juhudi za maendeleo vijijini nchini Rwanda

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani, WFP, Ertharin Cousin, leo amehitimisha ziara ya siku tatu nchini Rwanda, ambayo imekuwa kituo cha mwisho cha ziara yake barani Afrika, ambayo iliangazia masuluhu ya vijijini kwa matatizo ya njaa na utapiamlo.

Akiwa nchini Rwanda, Bi Cousin amekutana ana kwa ana na watu ambao wamekuwa wakipokea msaada wa WFP kwa njia mbalimbali, wakiwemo wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ambao wamemwambia kuwa bila msaada wa chakula wanachopokea kutoka kwa WFP kila mwezi ambacho kimekuwa tegemeo lao, wasingeweza kuishi.

Bi Cousin pia amekutana na raia wa Rwanda ambao wanajitahidi kujikwamua wenyewe na jamii zao kutoka katika umaskini kupitia miradi inayoangazia kupunguza utapiamlo wa mara kwa mara na kuongeza usalama wa chakula na riziki zao.

Mkuu huyo wa WFP ameisifu mikakati ya vijijini ambayo imewasaidia watu kuboresha viwango vyao vya maisha, na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano baina ya mashirika ya Umoja wa Mataifa, jamii na serikali katika kuwasaidia watu kujiondoa katika umaskini.