Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haki za binadamu ni muhimu katika mchakato wa amani Colombia:Pillay

Haki za binadamu ni muhimu katika mchakato wa amani Colombia:Pillay

Kuheshimu haki za binadamu itakuwa muhimu sana wakati Colombia ikipitia kipindi cha mpito kutoka vitani kuelekea kwenye amani, amesisitiza afisa wa haki za binadamu akiainisha kwamba hasa haki za waathirika lazima ziwe kitovu cha majadiliano baina ya serikali na  makundi ya waasi.

 Bi Navi Pillay kamishna mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa amesema haitokuwa rahisi kuunda taifa ambalo litaheshimu haki za kila mmoja baada ya miaka kadhaa ya vita.

Bi Pillay ametoa kuali hiyo kwenye mkutano na waandishi habari mjini Bogota wakati akihitimisha ziara yake.  

Serikali inakadiria kwamba watu 600,000 wamekufa tangu kuuanza kwa vita baina ya serikali na kundi la waasi la Revolutionary Armed Forces of Colombia (FARC)  katika miaka ya 1960.

Hivi karibuni pande hizo mbili zimekuwa zikijihusisha na majadiliano kuhusu masuala mbalimbali katika juhudi za kumaliza vita hivyo vya miongo mingi.

Pillay akiwa Colombia amekutana na Rais Juan Manuel Santos ambaye amesisitiza kutekeleza wajibu wake wa kuhakikisha mabadiliko katika haki za binadamu na kuleta amani .

Pia amekutana na viongozi wengine wa serikali, wawakilishi wa jumuiya za kijamii, watetezi wa haki za binadamu, waathirika wa vita, wakuu wa kanisa na wawakilishi wa sekta binafsi.