Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Twahitaji taarifa kuhusu viongozi wa Misri waliotiwa nguvuni: Pillay

Twahitaji taarifa kuhusu viongozi wa Misri waliotiwa nguvuni: Pillay

Ofisi ya Haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imesema wiki moja tangu kuiandikia waraka serikali ya mpito ya Misri ikitaka kufahamu misingi ya kisheria iliyosababishwa Rais wa zamani wa nchi hiyo Mohammed Morsi na maafisa wengine waandamizi wa serikali kuendelea kuwa nguvuni hakuna jibu lolote kutoka serikali hiyo ya mpito. Taarifa zaidi na Assumpta Massoi.

(Taarifa ya Assumpta)

Katika barua hiyo Kamishna Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Navi Pillay pamoja na kuhoji misingi ya kuendelea kutiwa nguvuni viongozi hao, pia anataka kupatiwa orodha kamili ya wale wote waliotiwa nguvuni tangu serikali iliyokuwa ikiongozwa na chama cha Muslim Brotherhood kuondolewa madarakani nchini Misri.

Halikadhalika anataka kufahamu iwapo kuna hati yoyote ya kukamatwa iliyotolewa ili kuendelea kuhalalishwa kushikiliwa kwao. Ofisi ya Haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa imesema barua hiyo iliandikwa wiki iliyopita lakini hadi sasa hakuna jibu lolote. Rupert Colville ni msemaji wa ofisi hiyo.

(SAUTI YA RUPERT)

Halikadhalika amesema Bi.Pillay pia ameomba kibali ili jopo la wachunguzi wa haki za binadamu liweze kuruhusiwa kwenda Misri kufuatilia hali ya haki za binadamu kwa sasa.