Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Siku ya Mandela ni wakati wa kuchukua hatua na kuyakumbuka aliyotenda:Ban

Siku ya Mandela ni wakati wa kuchukua hatua na kuyakumbuka aliyotenda:Ban

Watu duniani kote wanachagizwa kuchukua hatua kwa niaba ya wengine Alhamisi ya leo katika kusherehekea siku ya kimataifa ya Nelson Mandela.

Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Umoja wa MAtaifa Ban Ki-moon ambaye anaadhimisha siku hii kwa kukumbuka maisha na mchango mkubwa wa kiongozi huyo wa kimataifa ambaye kwa sasa bado yuko mahututi hospitali.

Siku ya kimataifa ya Nelson Mandela International inasherehekea siku ya kuzaliwa na miongo ya huduma iliyotolewa na Rais huyo wa zamani wa Afrika ya Kusini ambaye leo Julai 18 ametimiza miaka 95 .

Katibu Mkuu amesema wakati watu waki mtumia salamu za heri lakini pia waonyeshe hisia zao kwa kuitumia siku hii kufanya kazi za kujitolea kwa ajili ya wengine na kwa ajili ya dunia.

Baraza kuu leo lina kikao maalumu kisicho rasmi kwa ajili ya kumuenzi Mandela na miongoni mwa wazungumzaji ni Bill Clinton Rais wa zamani wa Marekani, mwanamuziki, muigizaji na mwana harakati Harry Belafonte, na Andrew Mlangeni, ambaye alifungwa pamoja na Mandela na mpaka sasa ni marafiki wakubwa.