Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afya barani Afrika itasaidia kuinua ukuaji wa uchumi:UNAIDS

Afya barani Afrika itasaidia kuinua ukuaji wa uchumi:UNAIDS

Ripoti iliyozinduliwa leo kwenye mkutano maalumu wa Muungano wa Afrika na kuhusu ukimwi, kifua kikuu na malaria imetanabaisha kwamba kuongeza fedha katika matumizi ya sekta za afya ni msingi muhimu katika ukuaji wa uchumi na maendeleo katika bara la Afrika.

Ripoti hiyo iitwayo “Abuja+12:uandaaji wa mustakhbali wa afya Afrika” imechapishwa na Muungano wa Afrika kwa ushirikiano na shirika la Umoja wa Mataifa la kupambana na ukimwi UNAIDS.

Ripoti hiyi imetathimini hatua zilizopigwa tangu azimio la Muungano wa Afrika AU la mwaka 2001 mjini Abuja ambalo liliwataka viongozi wa bara hilo kukusanya fedha ndani na nje kwa ajili ya kushughulikia masuala ya afya na kuondoa vikwazo vya vita dhidi ya ukimwi.

Pia ripoti imeeleza mapengo yaliyopo na masuala ya kuyapa kipaumbele na hatua za kuchukua. Ripoti imependekeza mambo matano ya kuwa na bara la Afrika lenye afya njema. Ambayo ni viongozi kuungana pamoja, kutafuta ufadhili, kuwekeza katika afya, kuboresha nguvu kazi na kuhakikisha hakuna atakayeachwa nyuma.