Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban amteuwa Phumzile Mlambo-Ngcuka wa Afrika Kusini kuwa mkuu wa UN Women

Ban amteuwa Phumzile Mlambo-Ngcuka wa Afrika Kusini kuwa mkuu wa UN Women

Kufuatia ushauriano na nchi wanachama, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon, ametangaza leo kuteuliwa kwa Phumzile Mlambo-Ngcuka wa Afrika Kusini kama Mkurugenzi Mkuu wa kitengo cha Umoja wa Mataifa kinachohusika na kuendeleza usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake, UN Women. Bi Mlambo-Ngcuka anachukuwa nafasi ya Bi Michelle Bachelet.

Bwana Ban ameelezea shukrani zake kwa Mkurugenzi anayeondoka kwa kujitolea kwake kuendeleza kazi ya Umoja wa Mataifa kuhusu usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake kwenye ngazi za kimataifa, kikanda na kitaifa, na kutolea sifa uongozi wake Bi Bachelet kama Mkurugenzi Mkuu wa kwanza wa Un Women.

Bi Phumzile Mlambo-Ngcuka ana uzoefu mkubwa katika kupigia debe masuala ya wanawake, pamoja na uzoefu katika usimamizi. Aliwahi kuwa mwanamke wa kwanza kabisa kushikilia wadhfa wa Makamu wa Rais wa Afrika Kusini, tokea mwaka 2005 hadi 2008. Aliwahi pia kuhudumu kama Waziri Msaidizi katika Wizara ya Biashara na Viwanda (1996-1999) na kama Waziri wa Madini na Nishati (1999-2005), na pia kama Waziri wa Sanaa, Utamaduni, Sayansi na Teknolojia mwaka 2004.