Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza Kuu lajadili mchango wa Umoja wa Mataifa katika uongozi wa kimataifa

Baraza Kuu lajadili mchango wa Umoja wa Mataifa katika uongozi wa kimataifa

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa leo limefanya mdahalo kuhusu azimio linalohusu mchango wa Umoja wa Mataifa katika uongozi wa kimataifa na pia kujadilia utekelezaji wa matokeo ya mkutano wa Rio+20 kuhusu maendeleo endelevu. Joshua Mmali amefuatilia mkutano wa leo

TAARIFA YA JOSHUA

Baraza hilo Kuu limeanza kikao chake kwa kutoa heshima kwa marehemu Stoyan Ganev, aliyekuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Bulgaria, na ambaye aliwahi kuwa rais wa kikao cha 47 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Akiongea mwanzoni mwa kikao cha leo, rais wa Baraza Kuu Vuk Jeremic, amesema tangu kupitishwa kwa azimio la Rio+20, hatua kadhaa zimepigwa katika kubuni ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015.

Katika kikao hicho, Baraza Kuu limepitisha azimio kuhusu wajibu wa Umoja wa Mataifa katika uongozi wa kimataifa. Bwana Jeremic amesema azimio hilo linajumuisha uwezeshaji wa mazungumzo baina ya Umoja wa Mataifa na nchi ishirini tajiri zaidi duniani, au G20, kupitia mikutano itakayoandaliwa na rais wa Baraza hilo, ili kuendeleza uwazi na utangamano, pamoja na kuimarisha uelewano na ushirikiano katika masuala ya kimataifa ya uongozi na kiuchumi.

Kwa kutoa jukumu kwa mataifa ya G20 katika kuyafikia maendeleo endelevu, azimio hili linaliongezea nguvu azimio la mkutano wa Rio+20, ambalo linasema kuwa maendeleo endelevu yanatakiwa yawe na mtazamo wa kimataifa na kuweza kutimizwa na nchi zote duniani.