Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali Sudan Kusini yamulikwa kwenye Baraza la Usalama

Hali Sudan Kusini yamulikwa kwenye Baraza la Usalama

Hapa mjini New York, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limekutana leo kwa ajili ya Sudan Kusini, wakati taifahilolinapojiandaa kuadhimisha miaka miwili tangu kujipatia uhuru wake hapo kesho. Joshua Mmali amekuwa akifuatilia(TAARIFA YA JOSHUA)

Mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini ambaye pia ni mkuu wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo, UNMISS, Bi Hilde Johnson, ameliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa, wakati taifa hilo linajiandaa kuadhimisha miaka miwili tangu kujipatia uhuru hapo kesho, kumeshuhudiwa changamoto na matatizo mengi ambayo yameanza kuuzima mwanga wa furaha ilokaribisha uhuru huo miaka miwili ilopita.

Licha ya changamoto na matatizo hayo, Bi Johnson amesema ni vyema kuzitambua hatua muhimu ambazo taifahilolimepiga kwenye mkondo wa kuweka utulivu na demokrasia tangu kupata uhuru, kwa msaada wa UNMISS. Amesema kumekuwa na marekebisho katika sekta ya usalama, hususan katika jeshi la polisi, uongozi wa kisheria na utekelezaji wa mkakati wa kujenga amani.

Bi Johnson amesema licha ya hatua hizi zilizopigwa, baadhi ya maeneo yamesalia nyuma, akitoa mfano wa jimbo la Jonglei kusini mashariki mwa nchi. Amesema kuzorota kwa hali ya usalama katika baadhi ya maeneo nchini humo kumeambatana na ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na makundi yenye silaha na vikosi vya usalama vya serikali. Bi Johnson amesema jukumu la ujumbe wa UNMISS ni kuisaidia Sudan Kusini kufanya marekebisho zaidi katika mifumo yake.

(CLIP HILDE)

"Mimi pamoja na wengine katika UNMISS, tunaahidi kuisadia serikali kupiga hatua katika kufanya marekebisho zaidi ya kisiasa, kutunga katiba, kuboresha hali ya haki za binadamu, na kufanya hesabu ya watu na uchaguzi wa kidemokrasia. Malengo haya yatasaidia kuhakikisha kuwa Sudan Kusini inasalia kwenye mkondo wa utulivu na maendeleo."