Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban apongeza jukumu la mabaharia katika kuchagiza biashara ya kimataifa

Ban apongeza jukumu la mabaharia katika kuchagiza biashara ya kimataifa

Leo ni siku ya mabaharia duniani ambapo Umoja wa Mataifa umetaka kuchagizwa kwa harakati za kuongeza idadi yao kwa mustakhbali wa biashara bora duniani. Alice Kariuki na taarifa zaidi.

(ALICE TAARIFA)

Bila mchango wa mabaharia milioni 1.5 duniani , biashara ya kimataifa itakuwa katika hatihati amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon. Katika ujumbe maalumu wa kuadhimisha siku ya mabaharia ambayo ni Juni 25 kila mwaka Ban amewataka watu kila mahali kufikiria kuhusu ujasiri wa wanawake na wanaume ambao hushughulikia kiwango kikubwa cha usafirishaji wa mizigo duniani.

Mojawapo ya vikwazo vya ubaharia ni uharamia. Philip Holihead anaongoza mradi wa kukabiliana na uharamia unaoendeshwa na shirika la kimataifa la masuala ya bahari (IMO) mjini Nairobi, Kenya, na amefanya kazi zaidi ya miongo mitatu na Royal Navy. Anasema mafanikio katika vita dhidi ya uharamia kwenye bahari ya Hindi yanaweza kupatikana kutokana na vigezo mbalimbali ikiwemo kuwaelimisha watu wanaofanya kazi melini.

(SAUTI YA PHILIP HOLIHEAD)

Kwanza ni kanda kutambua na uwezo lazima ujengwe, lakini pia kutovumilia na kufanya kazi pamoja. Lakini pia lazima tukumbuke jukumu la wanamaji wa kimataifa na nchi ambazo zimechangia meli za kimataifa za kushika doria kwenye bahari ya Hindi na Ghuba ya Aden. Na mwisho kwa mabaharia wenyewe, ambao wameandaliwa kwenda katika maeneo ya hatari ambako maharamia wamekuwa wakiendesha shughuli zao na kujimarisha kupitia kitu wanachokiita mpango mzuri wa udhibiti kwa kujihami dhidi ya meli zinazopita katika sehemu yao.

Hata hivyo William Walesa, mhadhiri mwandamizi katika Chuo cha ubaharia nchini Tanzania, DMI anasema uhaba wa mabaharia unatokana na ukiritimba wa kisheria.

(SAUTI WALESA)