Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kesi dhidi ya Uhuru Kenyatta yasogezwa mbele

Kesi dhidi ya Uhuru Kenyatta yasogezwa mbele

Hii leo Alhamisi huko The Hague, Uholanzi, Mahakama ya kimataifa ya makosa ya uhalifu, ICC imesogeza mbele hadi tarehe 12 Novemba mwaka huu siku ya kuanza kusikilizwa kwa kesi dhidi ya Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya. Kesi hiyo awali ilikuwa ianze kusikilizwa tarehe Tisa mwezi ujao.  Uamuzi huo unafuatia moja ya vitengo vya mahakama ya ICC tarehe 26 mwezi Aprili mwaka huu kuamua upande wa utetezi uongezewe muda zaidi wa maandalizi kwa kuwa upande wa mashtaka unachelewa kufichua ushahidi wake. Upande wa utetezi uliwasilisha maoni yake na muda unaoona unatosha kwa maandalizi ya kesi hiyo.  Mahakama ilipokea mapendekezo hayo pamoja na majibu kutoka upande wa mashtaka na wawakilishi wa wahanga kwenye kesi hiyo na ndipo majaji wakapanga tarehe 12 mwezi Novemba.

Bwana Kenyatta anakabiliwa na makosa matano ya tuhuma za kuhusika na vitendo vya uhalifu dhidi ya binadamu wakati wa vurugu za baada ya uchaguzi mkuu waKenyamwaka 2007/2008.