Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban amteua Kobler kuwa mwakilishi wa UM wa MONUSCO

Ban amteua Kobler kuwa mwakilishi wa UM wa MONUSCO

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Jumatatu ametangaza kwamba amemteua Martin Kobler raia wa Ujerumani kuwa mwakilishi wake maalumu wa mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (MONUSCO).

Mwakilishi huyo mpya atachukua nafasi ya Roger Meece kutoka Marekani ambaye atakamilisha muda wake Julai mwaka huu. Katibu Mkuu amesema anashukuru kwa kazi nzuri na huduma iliyotolewa na Bwana Meece katika kuusaidia mpango wa MONUSCO kutimiza majukumu yake.

Bwana Kobler ana uzoefu katika masuala ya kimataifa baada ya kuhudumu ofisi ya mambo ya nje kwa zaidi ya miaka 25 nchini mwake na kama afisa wa Umoja wa mataifa.

Kabla ya kuwa mkuu wa mpango wa Umoja wa Mataifa Iraq UNAMI bwana Kobler naibu mwakilishi maalumu wa mpango wa Umoja wa mataifa Afghanistan UNAMA kuanzia 2010 hadi 2011.

Pia alikuwa mkurugenzi mkuu wa kitengo cha utamaduni na mawasiliano katika wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani na pia balozi wan chi yake Iraq na Misri.

Bwana Kobler aliyezaliwa mwaka 1953 ana shahada ya sheria kutoka chuo kikuu cha Bonn Ujerumani, ameoa na ana watoto watatu.