Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mamluki wanachochea ghasia za kidini Syria: UM

Mamluki wanachochea ghasia za kidini Syria: UM

Baraza la haki za binadamu limekuwa na mjadala maalum hii leo huko Geneva kuhusu mzozo wa Syria ambapo Umoja wa Mataifa umesema ongezeko la mamluki wanaoingia nchini humo kusaidia vikosi vya serikali na wapinzani linachochea ghasia kwa misingi ya kidini na kuonya kuwa kitendo hicho kinaweza kutikisa utulivu wa eneo zima. George Njogopa na taarifa zaidi.

 (RIPOTI YA GEORGE NJOGOPA)

 Mkuu wa Kamishna ya haki za binadamu Navy Pillay amesema kuwa mzozo wa Syria unachochewa na pande mbili, kwa upande mmoja na serikali na kwingineko na makundi ya nje ambayo hushiri kwenye usambazaji wa silaha kwa makundi ya waasi.  Akizungumza kwenye Baraza Kuu la Haki za Binadamu ambalo limeitishwa maalumu kwa ajili ya kujadilia hali ya mambo yaSyria, Kamishna huyo amesema kuwa kuna haja kwa jumuiya ya kimataifa kuwa na sauti moja ili kumaliza hali hiyo ya mkwamo ambayo inawaathiri zaidi wananchi wa kawaida. Amesema kuwa, utanzuaji wa mzozo huo hauwezi kufaulu kwa kutumia mitutu ya bunduki lakini jambo linalopaswa kuzingatiwa sasa ni uanzishwaji wa mazungumzo ya kisiasa.

 (SAUTI YA NAVI PILLAY)

“ Tunapaswa kuweka tofauti zetu kando, na dola zenye ushawishi zinapaswa kutumia nguvu zao kuzuia utumiaji zaidi wa silaha nzito pamoja na uvurumishwaji wa mabumu ya angani katika maeneo ya raia. Mataifa yenye nguvu yanapaswa kuweka bayana misimamo yao ya kutoruhusu kuachilia mauaji zaidi pamoja na uharibifu ikiendelea. Baraza linapaswa kutuma ujumbe wa wazi kwa pande zote kwenye mzozo kusitisha mapigano na pande za nje zinazochochea hali hii zinapaswa kuacha mara moja. Mapigano hayo yanapaswa kusimama mara moja na kuanzishwa kwa ujenzi wa kuaminiana hasa wakati huu wa kuelekea kwenye kongamano la Geneva . Upelekwaji wa silaha lazima usimame, na uanzishwaji wa majadilino ya kitaifa unapaswa kuanza sasa”.