Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanawake kutoka jamii za watu wa asili Amerika Kusini wasalia nyuma kisiasa:UNDP

Wanawake kutoka jamii za watu wa asili Amerika Kusini wasalia nyuma kisiasa:UNDP

Utafiti uliotolewa na shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP inaonyesha kuwa Amerika ya Kusini katika miongo miwili iliyopita imejitahidi kuwajumuisha watu wa asili katika masuala mbalimbali ya kijamii lakini ushiriki wao katika masuala ya kisiasa na hususani wanawake bado ni mdogo mno.Ripoti hiyo imetolewa katika kongamano la 12 la watu wa asili linaloendelea kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York.

Ripoti hiyo inatokana na mchango wa ushiriki wa watu wa asili katika nchi sita za Amerika ya Kusini ambazo zina idadi kubwa ya watu wa asili na zilizopiga hatua kubwa katika ushiriki wa michakato ya kisiasa ambazo ni Bolivia, Ecuador, Guatemala, Mexico, Nicaragua na Peru.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo  kuna mambo muhimu yaliyowasaidia watu wa asili kushiriki katika siasa kwenye ukanda huo yakiwemo  ongezeko la watu wa asili kuhamia maeneo mengine ambapo wamefaidika na teknolojia ya mawasiliano,kamasimu za mkononi, tovuti na mitandao ya kijamii.

Pili kupanuka kwa wigo wa haki zao hasa baada ya nchi hizo kutia saini mikataba ya kimataifa kuhusu watu wa asili na tatu ni ongezeko la mashirika mengo ynayopigia chepuo masuala ya watu wa asili.

Hata hivyo ripoti hiyo inasema  ushiriki wa wanawake wa asili katika siasa imekuwa changamoto kubwa kwa sababu wanakabiliwa na ubaguzi mara tatu, kwanza kwa kuwa ni wanawake, pili watu wa asili na tatu kwa kuwa masikini.