Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Somalia yajadili ujenzi wa taifa kwa ufadhili wa wahisani

Somalia yajadili ujenzi wa taifa kwa ufadhili wa wahisani

Majadiliano ya ushiriki wa kutatua hali tete nchini Somalia

(SAUTI MJADALA)

Ni katika mkutano unaomkutanisha Waaziri Mkuu wa Somalia Abdi Farah Shirdon na wadau mbalimbali wakiwemo wahisani lengo ni ujenzi wa taifa sambamba na amani ya Somalia.

Huu ni makakati mahususi ulioasisiwa na nchi zilizoendelea kiviwanda G7 mnamo mwaka 2011 kwa ajili ya mageuzi ya muundo wa utoaji wa kimisaada wa kimataifa kwa Somalia nchi iliyokumbwa na migogoro kwa miongo kadhaa.

Mwenyeji wa mkutano huu Waziri Mkuu wa Somalia anasema

(SAUTI YA FARAH)

" Utoaji wa fedha za kutosha kwa  Somalia ni kusongesha shughuli za maisha na kutoa riziki ambako kutasaidia kufungua fursa za mchakato wa ujenzi wa kisiasa na kuimarisha misingi ya vipaumbele vya taifa na huu ni mwanzo wa kuweka misingi ya maendeleo endelevu”.

Wachambuzi wa mambo wanasema Chini ya makubaliano haya mapya yako matumaini makubwa ya kupiga hatua kiuchumi, kisiasa, kiusalama na hata kisheria  hasa ikizingatiwa kuwa tishio lililokuwa kubwa la kundi lenye msimamo mkali la Alshabaab limeondolewa katika sehemu kuu za Kusini na Kati mwa Somalia

Mjumbe maalum wa Umoja wa Ulaya nchini humo , Michele Cervone d'Urso anaiona Somalia yenye neema kwa siku za usoni.

(SAUTI YA MICHELE)

“Makubaliano mapya ni mchakato ulioongozwa na Somalia na kutekelezwa na Wasomali. Jumuiya ya Kimataifa inafuatailia kwa makini. Leo ilikuwa ni mwanzo wa mchakato huu wa muda mrefu  ambao pia utaelekea katika kongamano mwezi September mjini Brussel."

Kwa upande wake Mkurugenzi wa mpango wa maendeleo wa Umoja wa Mataifa David Clapp anachagiza mjadala huu kwa kusema

(SAUTI YA CLAPP)

" Umoja wa Mataifa unafurahia sana kusaidia mpango huu wa kuiwezesha Somalia kujiongoza yenyewe ambao unalenga katika kujenga imani na malengo matano ya ujenzi wa amani na jamii ya Wasomali ambayo imewakilishwa kwa ukubwa katika tukio la leo itafanya kazi pamoja."

Katika makubaliano haya kikosi kazi maalum kitafanya tathimini ya rasilimali zinazotakiwa, kuunda mfumo wa kuwajibika na usimamizi na kuunda mpango wa taifa wa maendeleo.