Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Visa zaidi vya maambukizi ya homa ya A(H7N9) vyaripotiwa China

Visa zaidi vya maambukizi ya homa ya A(H7N9) vyaripotiwa China

Wizara ya Afya na Tume ya Uzazi wa Kupanga nchini China imelifahamisha Shirika la Afya Duniani, WHO kuwa imethibitisha visa viwili zaidi vya maambukizi ya virusi vya homa ya A(H7N9).

Mgonjwa wa kwanza ni mwanamume mwenye umri wa miaka 69 kutoka mkoa wa Fujian, ambaye alianza kuumwa mnamo Aprili 29, naye mgonjwa wa pili na mvulana mwenye umri wa miaka 9 kutoka mkoa huo wa Fujian, ambaye alianza kuumwa mnamo Aprili 26 mwaka huu.

Halikadhalika, wagonjwa watano walioripotiwa awali wamefariki dunia. Kufikia sasa, vimeripotiwa jumla ya visa 130 vya maambukizi ya virusi vya homa ya A(H7N9) vilivyothibitishwa katika maabara, vikiwemo vifo 31. Watu waliokuwa karibu na wagonjwa walothibitishwa wanafuatiliwa kwa karibu, huku uchunguzi ukiendelea ili kubainisha chanzo cha maambukizi ya homa hiyo.

WHO haijatoa mapendekezo yoyote ya upimaji maalum wa watu kwenye vituo vya kuwasili nchi za kigeni, wala kupendekeza vikwazo vyovyote vya usafiri na biashara kutokana na hali hii.