Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hifadhi ya jamii ni muhimu katika kuondoa ajira kwa watoto

Hifadhi ya jamii ni muhimu katika kuondoa ajira kwa watoto

Shirika la kazi duniani, ILO limetoa ripoti inayoeleza bayana kuwa sera bora za hifadhi ya jamii ni nguzo ya kuondokana na ajira kwa watoto.

Ufafiti huo ulioangazia udhaifu wa kiuchumi, hifadhi ya kijamii na vita dhidi ya ajira kwa watoto ulihusisha nchi mbali mbali ikiwemo Tanzania, Botswana, Malawi na Namibia ambapo kipato miongoni mwa wazee kilionekana kuwa na uhusiano na ajira kwa watoto.

Mathalani, kiwango cha kipato cha mzee anayetunza wajukuu kinadhihirisha uwezo wa kudhibiti ajira kwa watoto. Huko Brazili, kiwango cha watoto kujitumbukiza kwenye ajira kimepungua hususan katika kaya ambazo zinanufaika na mfumo wa kupatiwa pesa kila mwezi kwa ajili ya kulipa karo za shule.

Mkurugenzi wa programu ya ILO ya kutokomeza ajira kwa watoto Constance Thomas amesema ripoti hiyo imetoa mwanga wa umuhimu wa kuwekeza katika hifadhi ya jamii jamii kama njia ya kutokomeza ajira kwa watoto ambapo pia inajumuisha watu wazima kupata kazi zenye staha na watoto kupata elimu.