Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Harakati za kudhibiti mabadiliko ya tabianchi zashika kasi

Harakati za kudhibiti mabadiliko ya tabianchi zashika kasi

Huko Bonn, Ujerumani mazungumzo yameanza hii leo chini ya sekretariati ya Umoja wa Mataifa inayohusika na masuala ya mabadiliko ya hali ya hewa, (UNFCCC), kuangalia hatua za kuchukua kudhibiti ongezeko la utoaji wa hewa chafuzi zinazoongeza kiwango cha joto duniani.Mkutano huo unalenga kujadili fursa mbali mbali kuelekea makubaliano kuhusu hali ya hewa yatakayofikiwa kwenye mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya hewa mwaka 2015 na jinsi ya kutekeleza mpango kazi uliopo wa kudhibiti mabadiliko ya tabianchi.

Katibu Mtendaji wa UNFCC Christiana Figueres, amesema ni matumaini yake kuwa mazungumzo hayo yatawezesha kubaini mambo ya msingi ya makubaliano hayo, ikiwemo mambo yanayohitajika ili yaweze kufanikiwa kama sehemu ya matokeo ya mkutano huo wa mwaka 2015.

Mathalani washiriki wataangalia sheria kuhusu hali ya hewa zinazotekelezwa na serikali mbali mbali, utoaji wa gesi chafuzi na biashara ya viwango vya gesi chafuzi, na jinsi gani jitihada za kutumia nishati endelevu zinaweza kuongezwa ili kupunguza viwango vya gesi zinazoharibu mazingira.